Saturday, 18 April 2015

VIJANA WATOTO 115 WANASWA MAZOEZI YA KARATE DODOMA ..>>

        

Jeshi la Polisi mkoani hapa limefunga vituo vitatu katika eneo la Nkuhungu baada ya kubaini uwepo wa watoto na vijana 115 kutoka mikoa 13, ikiwa ni pamoja na visiwani Zanzibar, waliokuwa wakilelewa kwenye mazingira hatarishi.

Hata hivyo, kubainika kwa watoto hao ni tofauti na matukio ya mkoani Kilimanjaro ambako Jeshi la Polisi lilibaini zaidi ya watoto 200 waliokuwa wamefungiwa kwa miaka takriban mitatu wakipewa mafunzo ya kisiri na hivyo kuibua hisia za ugaidi.
Katika tukio la Dodoma, polisi imesema inaendelea na uchunguzi kujua walichokuwa wakifundishwa vijana hao.
Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana, kamanda wa polisi wa Mkoa wa Dodoma, David Misime alisema watoto hao wanatoka katika mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Kilimanjaro, Mtwara, Kagera, Tanga, Tabora, Singida, Pwani, Lindi, Geita, Mwanza na Manyara.
Alisema baada ya kupokea taarifa ya uwepo wa watoto hao, walifika katika vituo hivyo saa 6:30 usiku jana na kukuta watoto hao wenye umri wa chini ya miaka 25.
“Polisi iligundua vituo vitatu katika eneo la Nkuhungu, Dodoma Mjini baada ya kupokea taarifa kwamba kuna nyumba ambazo zinaonekana kuingia watoto wengi na inawezekana siyo mazingira salama ya kuishi binadamu hasa watoto na wanachofundishwa huenda ni kinyume cha maadili,” alisema.
Kamanda Misime alisema katika vituo hivyo walipatikana jumla ya watoto 63 wenye umri wa chini ya miaka 18, wakati walio na vijana wenye umri wa kati ya miaka 18 na 25 walikuwa ni 52. Alifafanua kuwa kati ya watoto hao waliotoka Wilaya ya Kondoa mkoani hapa ni 50 wakati waliotoka wilaya za Dodoma Mjini, Chamwino na Mpwapwa ni watoto 26.
“Uchunguzi unaendelea na yeyote atakayeguswa na ushahidi kuwa amekiuka sheria atafikishwa mahakamani, wakiwemo wazazi walioruhusu watoto kuwa katika uangalizi ambao siyo wa kutosha kama sheria ya watoto ya mwaka 2009 inavyoelekeza,” alisema.
Pia alisema jeshi hilo linachunguza watoto hao walikuwa wakifundishwa kitu gani na kama walikuwa wakihudhuria shule kulingana na umri wao na sheria za nchi zinavyoelekezwa.
Ingawa hakulihusisha tukio hilo na mafunzo ya ugaidi, Kamanda Misime aliwataka viongozi na watu wataka maeneo kama hayo katika himaya zao na vituo visivyosajiliwa ambavyo ni hatarishi kwa watoto, watoe taarifa mapema.
Pia alitoa wito kwa familia, viongozi wa serikali za mitaa, dini na taasisi nyingine kutoruhusu watoto wao kupelekwa na kuelelewa katika vituo hatarishi.
Aidha, aliwataka wazazi wanaofahamu watoto hao wajitokeze ili kupewa maelekezo kabla ya kutafutwa na mkono wa dola.

No comments:

Post a Comment