WACHIMBAJI wadogo wa dhahabu mkoani Shinyanga, maarufu ‘manyani’,
wamekufa katika machimbo madogo ya Kalole wilayani Kahama, baada ya
kufukiwa na kifusi usiku wa kuamkia jana.
Vifo hivyo vilitokana na mvua zinazoendelea kunyesha. Akizungumza kwa
simu, Mkuu wa Wilaya ya Kahama, Benson Mpesya alisema wachimbaji hao
walikumbwa na mauti hayo baada ya kuingia ndani ya mashimo hayo kwanjia
ya panya kwa lengo la kutafuta mawe yenye dhahabu.
Mpesya alisema wachimbaji hao ni wale ambao huingia mashimoni kuiba
mawe hayo, baada ya muda kumalizika wa kufanya kazi ambayo kwa kawaida
huishia saa 12.00 jioni.
Baada ya hapo, imeelezwa ndio watu hao ‘manyani’ huvamia mashimo hayo
nyakati za usiku kwa kuiba mawe hayo. Katika tukio hilo, Mpesya
(pichani) alisema wachimbaji hao wote 19 waliingia kwenye mashimo
manane, ambayo yameunganika kwa chini, walikufa baada ya mashimo hayo
kuanza kubomoka kutokana na mvua hiyo.
Mkuu huyo wa wilaya alisema baada ya ajali hiyo, kazi ya kufukua
ilifanyika ambapo maiti 19 waliopolewa ingawa kutokana na hali ya unyevu
kwenye mashimo hayo yanayoendelea kutitia, wamelazimika kusimamisha
ufukuaji.
“Unajua hawa ndugu zetu ni wale wachimbaji wasiokuwa na mashimo ambao
muda ukiisha wa kazi huingia kwenye mashimo hayo bila kuangalia usalama
na ndivyo ilivyotokea kwa wachimbaji hao,” alisema Mpesya na kuongeza
kuwa maiti 17 kati 19 wametambuliwa na ndugu zao.
“Tunasubiri wenzetu kutoka mgodi wa Bulyanhulu waje waone kwanza
mitambo ipi ambayo inaweza kutumika kufukua mashimo hayo, kwa kuwa
ufukuaji wa kienyeji tuliokuwa tukiutumia tumeusimamisha kutokana na
mashimo hayo kuendelea kutitia,” alisema Mpesya.
No comments:
Post a Comment