Bill Gates anuia kuyapiga vita maradhi
Gazeti la "Die Zeit " linatuarifu juu ya dhamira ya tajiri mkubwa
duniani, Bill Gates ya kuwasaidia masikini.Gazeti hilo linauliza jee
tajiri huyo ataweza kweli kuwaepusha masikini na maradhi ya hatari?
Gazeti hilo linakumbusha kwamba mkutano juu ya kile kinachoitwa
mfungamano wa chanjo za kukinga maradhi, Gavi ulifanyika hivi karibuni
mjini Berlin. Mwenyeji wa mkutano alikuwa Kansela wa Ujerumani Angela
Merkel.
Gazeti la "Die Zeit" linasema viongozi kutoka nchi mbalimbali hasa za
Afrika pia walikuwapo kwenye mkutano huo.Lakini mgeni muhimu kabisa
hakuwa kiongozi wa nchi yoyote, na wala halikuwa Shirika la Afya
Duniani, WHO, bali ni Wakfu wa Bill na Melinda Gates.
Gazeti la "Die Zeit" limearifu kuwa kuanzia mwaka ujao hadi mwaka 2020
Wakfu wa Bill na Melinda Gates utatoa dola Bilioni saba na nusu kwa
ajili ya kuutekeleza mradi wa chanjo, maarufu kama Gavi katika nchi za
Afrika.
Lengo la Wakfu wa Bill na Melinda, linasema gazeti la "Die Zeit" ni
kupambana na umasikini,maradhi na vifo vya mapema.Lakini gazeti hilo
limeuliza jee tajiri mmoja peke yake ataweza kupambana na maadui hao
wakubwa wa binadamu?
Mwandishi:Mtullya Abdu. Deutsche Zeitungen.
Mhariri: Josephat Charo
No comments:
Post a Comment