Monday, 11 May 2015

MIAKA 70 BAADA YA WW II VITA YA PILI YA DUNIA >>

Dunia imeadhimisha miaka 70 ya kumalizika kwa Vita vya Pili ya Dunia baada ya Jeshi la Kinazi la Ujerumani kujisalimisha kwa jeshi la muungano wa Jamhuri za Kisovieti, Mei 8, mwaka 1945.
Gwaride la kuadhimisha sherehe hizo lilifanyika Jumamosi mjini Moscow na viongozi 20 duniani walihudhuria, akiwamo Ban Ki-moon, Rais Xi Jinping wa China na Rais Raul Castro wa Cuba.

Maadhimisho hayo yamepewa jina la ‘siku ya kumbukumbu na maridhiano’,  huku mvutano kati ya Urusi na nchi za Magharibi ukiendelea kuhusu mzozo wa Ukraine.
Kutokana na kuwapo kwa mzozo huo, nchi za Magharibi zimesusia sherehe hizo mjini Moscow licha ya Urusi kutoa mchango  mkubwa wa kumaliza vita hivyo.
Katika mji wa Berlin, Bunge la Ujerumani liliiadhimisha siku hiyo baada ya jeshi lake kujisalimisha bila masharti.
“Mei 8, mwaka 1945 ilikuwa siku ya ukombozi barani Ulaya. Tunaomboleza leo baada ya mamilioni ya watu kupoteza maisha kwenye vita hivyo wakiwamo Wayahudi wa Ulaya,” alisema Spika wa Bunge la Ujerumani, Norbert Lammert.
Spika huyo aliwalaumu raia wa Ujerumani kwa kumuunga mkono Adolf Hitler katika vita hiyo.
Spika Lammert alisema: “Siku ya leo si siku ya ukombozi wa Ujerumani tu bali maadhimisho haya yanakumbusha majaribio machache yaliyofanywa na baadhi ya Wajerumani ya kutaka kumuua Hitler na waliofanya majaribio hayo wanapaswa kupongezwa  na kutukuzwa.  Maadhimisho hayo yalihudhuriwa na Kansela Angela Merkel na maofisa kadhaa wa ngazi za juu wa Ujerumani.
Wakati huohuo, sherehe hizo pia, zilifanyika Poland jana katika mji wa Gdansk na kuhudhuriwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa (UN), Ban Ki-moon, Rais wa Umoja wa Ulaya (EU), Donald Tusk na rais wa Ukraine. Pia, nchi nyingine za Ulaya ya Mashariki zilihudhuria maadhimisho hayo. Mji huo ni wa kwanza kwa raia wake kuathirika na vita hivyo chini ya majeshi ya Kinazi, mwaka 1939.
Vita vya Pili ya Dunia ilianza baada ya wanajeshi wa Ujerumani kuingia Poland Septemba 1939 na kumalizika Mei 8, 1945 baada ya Mkuu wa majeshi wa Ujerumani, Wilhelm Keitel, kusaini waraka wa kujisalimisha usiku wa manane kwenye makao makuu ya Jeshi la Kisovieti mjini Berlin.

Licha ya kuwapo kwa makubaliano ya kumaliza vita barani Ulaya, mgogoro huo uliendelea barani Asia hadi Agosti 1945.

No comments:

Post a Comment