
Waziri Mkuu mstaafu na mbunge wa Monduli, Edward Lowassa amesema umefika wakati kwa Tanzania kukimbia kwa kasi ili kukabiliana na changamoto kubwa ya maendeleo ya sayansi duniani.
Akihutubia katika sherehe za jubilee ya miaka 25
ya uaskofu na 40 ya upadri ya Askofu Paul Ruzoka katika Jimbo Kuu
Katoliki Tabora jana, Lowassa alisema maendeleo hayo yanapaswa yawe
darasa la kuirejesha Tanzania katika falsafa ya elimu ya kujitegemea.
“Elimu ya kujitegemea inajenga misingi imara kwa
wahitimu wanaomaliza shule kuendelea na masomo, kujiajiri au kuajiriwa
katika sekta mbalimbali,” alisema na kuongeza kuwa elimu ya Tanzania
inakabiliwa na changamoto nyingi.


Lowassa alilipongeza Kanisa Katoliki kwa mchango
mkubwa linaloutoa katika maendeleo ya elimu nchini kwa kusaidia
kupambana na ujinga, umaskini na maradhi.
Katika hatua nyingine, Lowassa aliliomba kanisa kushirikiana na Serikali na wananchi katika suala la ulinzi na usalama.
Lowassa alisema sasa kuna viashiria vya kuvurugika
kwa amani, huku akikumbushia matukio ya kushambuliwa kwa nyumba za
ibada visiwani Zanzibar na mkoani Arusha.
“Jukumu la ulinzi ni letu sote, kwa hiyo kanisa
nalo lina wajibu wa kuwakumbusha waumini wake kila wakati kutambua
wajibu wa kila mmoja kuwa mlinzi wa ulinzi na usalama wa nchi.
“Baba Askofu ningependa pia kuchukua fursa hii
kukuomba uendelee na juhudi za kuombea amani kwa ndugu zetu wa Burundi
kwa kuwa hali ya huko sasa imeanza kuchafuka,” alisema Lowassa.
Rais wa Baraza la Maaskofu Tanzania (TEC),
Mhashamu Askofu Tarcius Ngalalakumtwa alisema Askofu Ruzoka amefanya
kazi kubwa kuhakikisha amani inatamalaki nchini na nje ya nchi.
Sherehe hizo zilihudhuriwa na viongozi mbalimbali wakiwamo wabunge Profesa Athman Kapuya na Magreth Sitta.
No comments:
Post a Comment