Thursday, 7 May 2015

ASKARI WETU WAWILI WAMEUWAWA WAKILINDA AMANI CONGO ...>>

Askari wawili wa Tanzania waliokuwa kwenye kikosi cha kulinda amani Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), wameuawa na wengine 13 kujeruhiwa usiku wa kuamkia jana baada ya msafara wao kushambuliwa kwa roketi na waasi.

Tukio hilo linafanya idadi ya wanajeshi wa Tanzania waliouawa nchini humo kufikia watatu baada ya askari mwingine, Khatibu Mshindo kuuawa Agosti 2013 katika shambulio la bomu lililofanywa na waasi wa kikundi cha M23 kwenye Mji wa Goma ulioko Mashariki mwa DRC.
Wakati Mshindo, ambaye alikuwa miongoni mwa askari wa Tanzania wanaounda Jeshi la Umoja wa Mataifa akifikwa na mauti, wapiganaji wengine 10 walijeruhiwa.
Msemaji wa Mpango wa Kulinda Amani wa Umoja wa Mataifa DRC (Monusco), Felix Basse alikaririwa na Shirika la Habari la AFP akisema mashambulizi ya juzi yalifanyika katika Kijiji cha Kikiki kilichoko kilomita 37, kaskazini - Mashariki mwa Mji wa Kivu katika Kitongoji cha Beni. Askari wengine wanne hawajulikani waliko.
Alisema mbali na kupigwa na roketi hilo, pia kulikuwa na mashambulizi ya risasi. Hata hivyo, haikufahamika mara moja askari wangapi wamejeruhiwa na msako mkali unaendelea.

 
Alipoulizwa kuhusu tukio hilo, msemaji wa JWTZ, Joseph Masanja alisema: “Hizo habari ndiyo nimezisikia, ngoja nizifanyie kazi... siwezi kusema au kukupa habari nusu, tunataka tujue ilikuwaje, ilitokea nini, kivipi ndipo tutasema.”
Habari zilizopatikana baadaye jana, zilidai kuwa kutokana na mashambulizi hayo kuwa mazito, raia wa eneo hilo wamekimbilia porini na wengine kuomba hifadhi kutokana na wasiwasi wa mashambulizi hayo yaliyotokea umbali wa kilomita sita kutoka Mji wa Oicha kuendelea.
Mashambulizi hayo yalifanyika wakati askari hao wakiwa katika doria ya kawaida usiku na inaelezwa kuwa ni kulipiza kisasi baada ya askari 16 wa Kundi la Allied Democratic Forces (ADF), kuuawa katika mashambulizi makali mwishoni mwa wiki.
Kikosi hicho cha Tanzania kinachounda Jeshi la Umoja wa Mataifa, kinashirikiana Jeshi la Serikali la FRDC kukabiliana na waasi hao wanaodaiwa kutoka Uganda wanaounda Kundi hilo la ADF ambalo linaendesha vitendo vya uasi, mauaji na utekaji nyara Kaskazini Mashariki mwa DRC.
Hata hivyo, baada ya mashambulizi hayo, askari wa FRDC kwa kushirikiana na baadhi wa Tanzania, walianza kufanya msako mkali kuwakamata waliohusika.
Mkuu wa Misheni ya Monusco, Martin Kobler alisema jana kuwa wamechukizwa na mashambulizi ya mara kwa mara yanayotokea na hasa mauaji ya askari wa kulinda amani na raia.
“Ninalaani mashambulizi kwa askari wa Tanzania waliokuwa na kazi ya kulinda amani kwa raia wa Beni. Natuma salamu zangu za rambirambi kwa familia za wapiganaji hawa, majeruhi wapone haraka,” alisema Kobler.

No comments:

Post a Comment